Nijile kwenu wavyele, mpate kunitambiya,
Na ninyi wazungupole, kwenu nataka sikiya,
Yalo kuwa siku zile, niyaonayo ni yaya,
Kama yale ndiyo haya, yeshakuwa yaleyale.
Ni kiza kinizingile, sioni jema na waya,
Hawaza hapa na pale, niko katika ruwiya,
Naomba mniambile, iniondoke kayaya,
Kama yale ndiyo haya, yeshakuwa yaleyale.
Nauza kuno ni mbele, ama nyuma niambiya,
Si wene niyawazile, niyaonayo mapiya,
Usasa ama ukale, pandani nimebakiya,
Kama yale ndiyo haya, yeshakuwa yaleyale.
Natumbuza wanenile, kwamba zino ndiyo niya,
Na vyao vipaumbele, neno litapo timiya,
Wametusoza kusile, au hayakuningiya,
Kama yale ndiyo haya, yeshakuwa yaleyale.
Msambe nina uwele, ugwe mkaja nitiya,
Mambo hayendi mile, idhala imeningiya,
Kiwa huko ndiyo kule, nimesha potezwa ndiya,
Kama yale ndiyo haya, yeshakuwa yaleyele.
Simba akimla mwele, wazima mtafatiya,
Tahadhari muitwale, nga kwa kuchunguliya,
Kiwa hili ndiyo lile, awali mganambiya,
Kama yale ndiyo haya, yeshakuwa yaleyele.
Hapano nitamatile, nudhumu natamatiya,
Walokuwa na upele, kucha tumewapatiya,
Nilipo sipajuile, majibu nasubiriya,
Kama yale ndiyo haya, yeshakuwa yaleyale.
©MKANYAJI
HAMISI A.S KISSAMVU
0715311590
kissamvujr@gmail.com
kutoka (Baitu shi’ri)
MABIBO * DSM.(🇹🇿)
2-11- 2022
Maoni Mapya