Mimi nakataa

  1. Kwa kweli ile sauti,
    mjini ilotangaa
    kwamba tusile chapati
    piya nyingine bidhaa
    kwangu ni suala nyeti,
    na tena ninashangaa
    kisa ni yule jamaa
    mimi mtanisamehe
  2. Siachi kula andazi,
    na chapati za kung’aa
    unga wala siulizi,
    nikipewa nitatwaa
    hilo jambo siliwezi
    niache vyakunifaa
    kisa ni yule jamaa
    mimi mtanisamehe
  3. Siwezi kuacha kazi,
    penzi hilo kwangu laa
    wana wakose mavazi,
    wavalishwe vitambaa
    niyakose matumizi
    eti ndio ushujaakisa ni yule jamaa
    mimi mtanisamehe
  4. Siungi hayo maneno
    kipembeni ninakaa
    nipewe kilo ya ngano
    nijidai kushupaa
    hili siungi mkono
    hafanyi hata kichaa
    kisa ni yule jamaa
    mimi mtanisamehe
  5. Tuzisuse biashara
    kisa yule kuambaa
    kwangu hii si busara
    suseni mie nakaa
    mawazo haya si bora
    yatupwe yana kinyaa
    kisa ni yule jamaa
    mimi mtanisamehe
  6. Tamati ya beti sita
    nawaaga ulamaa
    mimi siachi mafuta
    wala sitoacha mbaa
    hili halikunivuta
    uadui tunazaa
    kisa ni yule jamaa
    mimi mtanisamehe.

Author: Gadi Solomon